Kahama
JESHI la Polisi mkoani Shinyanga linaendesha msako mkali wa kuwasaka watu au mtu waliohusika na kifo cha mwenyekiti wa kitongoji cha Igudijo wilayani Kahama Bw. Enos Banyanda (65) aliyeuawa kikatili kwa kuchomwa na kitu chenye ncha kali kichwani.
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Bw. Hussein Kashindye alisema mbali ya wauaji hao kumuua kikatili mwenyekiti huyo wa kitongoji pia walimfunga kamba shingoni na kuuning’iniza mwili wake juu ya dali ndani ya jengo ambalo halijakamilika ujenzi wake ili watu waamini alikuwa amejinyonga.
Kamanda Kashindye alisema mwili wa Bw. Banyanda uligunduliwa juzi saa 9.00 alasiri na wanakijiji ukiwa ndani ya jengo lililokuwa jirani na makazi yake baada ya siku tatu tangu alipotoweka nyumbani kwake.
Alisema siku tatu kabla ya kubainika kuwa Bw. Banyanda alikuwa ameuawa aliondoka nyumbani kwake kwa lengo la kumsindikiza baba yake mzazi aliyekuwa akirejea nyumbani kwake na kwamba baada ya hapo hakuweza kurejea tena nyumbani.
Kamanda Kashindye alisema mara baada ya taarifa za kupatikana kwa mwili wa Bw. Banyanda kupatikana, polisi walikwenda katika eneo la tukio na kuukuta mwili wake ukiwa umefungwa kamba shingoni na kuning’inizwa juu ya dali, lakini hata hivyo polisi waliokota kofia yake iliyokuwa imetupwa jirani.
“Hii kofia ya marehemu ilipookotwa ilikutwa ikiwa na damu nyingi, hali hii ilisababisha polisi wauchunguze vyema mwili wa marehemu ukiwa unaning’inia pale juu, ndipo katika uchunguzi huo walibaini alikuwa amechomwa na kichwani na kitu chenye ncha kali na kusababisha kifo chake,"
"Hawa wauaji waliamua kumfunga kamba na kumning’iza juu ili kupoteza lengo wananchi waelewe kuwa alikuwa amejinyonga wakati sivyo, hata eneo jirani na alipokutwa amening'inizwa palikuwa na dalili za miburuzo hali iliyoonesha wazi kabla ya kufanyika kwa mauaji palitokea purukushani za hapa na pale,” alieleza Bw. Kashindye.
Alisema hivi sasa polisi inaendelea na uchunguzi juu ya kifo hicho pamoja na kuendesha msako mkali wa kuwasaka wahusika wa mauaji hayo na kwamba hakuna mtu anayeshikiliwa.
Katika tukio lingine mkazi wa kitongoji cha Magata kijiji cha Bugandika Manispaa ya Shinyanga, Bw. Emmanuel Mlima (36) amekufa baada ya kujinyonga kwa kutumia kamba ya katani.
Kamanda Kashindye alisema tukio hilo lilitokea juzi huko katika kijiji cha Bugandika saa 2.00 asubuhi ambako wanakijiji waligundua mwili wa Bw. Mlima ukiwa unaning’inia juu ya mti akiwa amekufa baada ya kujinyonga.
Alisema uchunguzi wa awali umebaini kuwa huenda Bw. Mlima alifikia uamuzi huo wa kujitoa uhai kutokana na ugomvi wa kifamilia kati yake na wazazi wake, na kwamba polisi inaendelea na uchunguzi zaidi ili kuweza kubaini chanzo halisi kilichosababisha mwananchi huyo kuchukua uamuzi huo.
No comments:
Post a Comment